Shirika la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO), la Umoja wa Mataifa (UN) limefanya utafiti na kugundua kwamba Ongezeko kubwa la idadi ya watu limechangia upungufu wa maji safi duniani kwa kiasi kikubwa.
Hivyo limesema Serikali zinalazimika kutegemea zaidi usimamizi wa maji safi ili kuhakikisha afya ya jamii inaimarishwa na kukidhi mahitaji ya idadi ya watu duniani inayoongezeka haraka.
Tafiti hizo zimewasilishwa katika kongamano la maji la kimataifa lililofanyika huko nchini Brazili.
Imeelezwa kuwa mahitaji ya maji yanaongezeka kwa asilimia 1 kwa mwaka, hata wakati mabadiliko ya tabia nchi, uchafuzi wa hali ya hewa na mmomonyoko wa ardhi unatishia ubora wake na kupatikana kwake.
Hata hivyo mpaka sasa nchi nyingi zimekuwa zikitegemea usimamizi asilia wa mifumo ya maji uliotengenezwa na mwanadamu, kama vile hifadhi za maji, mikondo ya umwagiliaji na mitambo ya kusafishia maji.